Wednesday, May 16, 2012

OBAMA AWAKUBALI MASHOGA

Mwandishi Wetu

MAREKANI imeungana na Uingereza kushinikiza kutambuliwa kwa haki za mashoga, ikitumia rungu la misaada yake inayotoa kwa nchi mbalimbali duniani, huku ikitenga Dola za Marekani 3 milioni sawa na Sh5.1bilioni, kwa ajili ya kufanikisha mkakati huo.

Shinikizo hilo la Marekani ambalo ni taifa kubwa kiuchumi duniani, linazidi kuchochea mjadala ulioibuliwa na  Waziri Mkuu wa Uingereza, David Cameron, ambaye alitangaza katika mkutano wa Jumuiya ya Madola uliofanyika Uswis hivi karibuni kwamba,  nchi yake itasitisha misaada kwa nchi zote duniani ambazo hazitambui haki za mashoga.

Baada ya Cameron, Rais Barack Obama wa Marekani naye juzi alitangaza kwamba, taifa hilo kubwa litatumia uwezo wake wote ikiwamo misaada inayotoa kwa nchi mbalimbali kuhakikisha haki za mashoga zinatambuliwa na kuthaminiwa duniani.

Rais Obama alitoa msimamo huo jijini Washington katika hafla ambayo pia ilihudhuriwa na Waziri wa Mambo ya Nje wa Nchi hiyo , Hillary Clinton ambaye ndiye alikuwa mzungumzaji mkuu.

“Wengine wanasema kuwa haki za mashoga na haki za binaadamu ni vitu tofauti na havifanani, lakini ukweli ni kwamba ni kitu kimoja na chenye usawa,”alisema Clinton wakati akisoma taarifa hiyo maalumu yenye baraka za Obama.

Clinton alisema, “Tayari tumetenga kiasi cha Dola za Marekani 3 Milioni kwa ajili ya programu ya kutangaza haki za mashoga ili kuondokana na ubaguzi na unyanyasaji dhidi yao.”

Waziri huyo wa mambo ya nje, alisema  mpango huo unazitaka nchi ambazo sheria zake bado hazitambui haki za mashoga na kubadilisha sheria hizo ili jamii hiyo ya watu ianze kutambulika.

“Kwa nchi ambazo watu wanafungwa, kupigwa kutokana na kuwa mashoga ni muhimu viongozi wa nchi hizo, kuangalia jinsi gani wanaweza kukiangalia kikundi hicho cha watu. Si kwamba mashoga hawafanyi makosa, wanaweza kufanya au kutokufanya kama watu wa kawaida, lakini isiwe ni kosa la jinai mtu kuwa shoga,”alisema.
Kwa mujibu wa Clinton, haki za mashoga ni haki za kimataifa. "Hazina tofauti na haki za binadamu zilizotambuliwa na nchi 48 lililotolewa baada ya Vita Kuu ya Pili ya Dunia.

Naibu Msemaji wa Baraza la Usalama la Marekani, Caitlin Hayden alisema Serikali ya nchi hiyo si kwamba itapunguza au kuzuia misaada yake ya kimataifa ili kubadilisha utamadini wa nchi nyingine, bali inataka kuhakikisha haki za mashoga zinapewa pia kipaumbele.

Hii ni mara ya kwanza kwa Rais Obama kujitokeza hadharani na kutetea haki za mashoga, lakini aliwahi kupitisha sera iitwayo “ don’t ask, don’t tell” ikimaanisha “usiulize, usiseme” ambayo inawazuia mashoga kujiunga na kufanya kazi za jeshi kwa uwazi.

Mmoja wa viongozi wa Republican ambaye atawania nafasi ya Urais, Gavana Rick Perry alisema Obama kwa mara nyingine amewakosea Wamarekani kwa aina tofauti ya maisha yao kwa kuingiza aina hiyo ya maisha kitu ambacho mtu kama yeye Perry hawezi kukifanya.

Kauli hiyo ya viongozi wa Marekani inaonekana kuungana na ile iliyotolewa na  Cameron aliyesema, "Hii ni moja ya vitu vinavyoongoza sera yetu ya misaada kwa mataifa mbalimbali na tayari tumeanza kuitekeleza katika maeneo kadhaa.